MMILIKI WA BLOG HII

MMILIKI WA BLOG HII
TANGAZA NASI MATANGAZO YA KIJAMII BURE KUPITIA BLOG HII

Jumamosi, 11 Aprili 2015

Mgomo wa madereva watikisa nchi nzima.

                                      Mgomo wa madereva. 
Mabomu yarindima kituo cha mabasi ubungo, Serikali yasalimu amri, yaafikiana nao, Baadhi ya mabasi yalianza safari mchana.
 Wakati Mgomo wa mabasi umetikisa nchi nzima, mabomu ya machozi na risasi za moto jana zilirindima katika Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani, Ubungo, jijini Dar es Salaam na kusababisha taharuki kwa mamia ya wasafiri waliokuwepo kituoni hapo wakisubiri hatma ya safari zao.
 
Taharuki hiyo ilitokana na madereva wa mabasi yaendayo mikoani kugoma kufanya safari zao, baada ya serikali kuwataka kutimiza masharti iliyowapa yakiwamo ya kwenda kusoma kila baada ya miaka mitatu wanapokwenda kuhuisha leseni zao.
 
Hata hivyo, mgomo huo ulisitishwa saa 7 mchana na madereva kuanza safari  kuelekea mikoani, baada ya serikali kufuta sharti la kuwataka madereva kurudi shule na utumiaji wa tochi barabarani.
 
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka, alilazimika kutoa tamko hilo baada ya kikao chake na madereva  na viongozi wengine wa serikali.
 
HALI KABLA YA KUTOLEWA TAMKO
Wakati wasafiri wakiwa katika hali ya sintofahamu, ghafla kikosi cha kutuliza ghasia kilifika nje ya kituo hicho na kuanza kupiga mabomu ya machozi yalisababisha baadhi ya wasafiri wakiwamo watoto kupoteza fahamu na wengine kutapika.
 
Katika purukushani hizo, wananchi waliokuwa nje ya kituo hicho wakiwamo abiria na wasindikizaji, walianza kujibu mapigo kwa kuwarushia askari hao mawe na kuchoma moto matairi.
 
Mapambano hayo yaliyoanza saa 3:00 asubuhi na kudumu takribani saa moja, yalitulia baada ya kikosi hicho kuongeza nguvu zaidi kwa kuleta gari la maji ya washawasha pamoja na mengine yaliyokuwa na askari wenye silaha za moto na mabomu ya machozi.
 
WANANCHI WAOKOTA MABOMU
Wakati jeshi hilo likipiga mabomu hayo, baadhi yalikuwa hayalipuki na kudondoka chini.
 
mwandish Jumamosi ilimshuhudia kijana mmoja aliyekuwa nje ya mlango wa kutokea kituoni hapo, akiokota mabomu hayo na kuyaweka mfukoni kisha kuingia nayo mtaani.
 
Mmoja wa askari waliokuwa wakiyarusha alipoulizwa na mwandishi wa habari hizi, alisema kuwa endapo mtu huyo akiyatoboa  yatalipuka na kumletea madhara.
 
KAMANDA KOVA
Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova, aliwasili kituoni hapo huku akisindikizwa na magari yaliyokuwa yamesheheni askari polisi na kupokelewa na madereva hao kwa wimbo uliokuwa ukimtaka awaachie huru wale wote waliokamatwa baada ya kusitisha safari.
 
Kamanda Kova alikubaliana na madereva hao na kuwatangazia kuwa, amewaachia huru wale wote waliokamatwa maeneo tofauti jijini Dar es Salaam na kwingineko na kuagiza ufanyike utaratibu wa kuwafikisha hapo.
 
Kabla ya tangazo hilo, jeshi hilo lilikuwa limeshaachia huru viongozi wakuu ambao ni Mwenyekiti wa Muungano wa Umoja wa Vyama vya madereva nchini, Clement Masanja, Katibu wa Chama cha Mabasi, Abdallah Bubala, Katibu wa Umoja wa Madereva na Katibu wa Chama cha Malori, Rashid Salehe na Mjumbe wa Baraza la Umoja wa Madereva, Moris Liumbi.
 
MADERAVA NA  MAKONDAKTA WA DALADALA
Wengine ambao walikuwa hawajaachiwa ambao Kova alishinikizwa na madereva hao atekeleze hilo ni pamoja na watu 20 wakiwamo madereva na makondakta wa daladala waliokuwa wanashikiliwa kituo cha Buguruni.
 
Pia wapo madereva wa mabasi ya mikoani 25 waliokuwa wamekamatwa wakati wakiwa safarini kuja Dar es Salaam wakitokea Morogoro na kiongozi mmoja wa madereva wa mkoa wa Iringa.
 
Baada ya kauli ya Kova, ilipotimu saa 5:49 asubuhi baadhi ya wale waliokuwa wanashikiliwa na jeshi hilo, waliwasili kituoni hapo huku madereva wakiimba wimbo wa kumsifu mkuu huyo wa polisi Dar es Salaam.
 
Hata hivyo, licha ya jitihada hizo za jeshi la polisi za kuwaachia huru watu hao, madereva hao walikuja na hoja nyingine ya kumtaka kamanda Kova, kuwaleta viongozi wa serikali hapo ili wazungumze nao kuhusu kero zao.
 
Kamanda Kova alichukua kipaza sauti na kuwaeleza kuwa, tayari ameshawasiliana na Waziri wa Kazi na Ajira, Kabaka ambaye alikubali ombi hilo.
KABAKA AWASILI
 
Saa 6:16 mchana Waziri Kabaka alifika akiongozana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki.
 
Viongozi wengine waliofika ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dk. Shaaban Mwinjaka na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda.
 
MADAI YA MSINGI YAKUBALIWA
Mkutano ulianza kwa Katibu Salehe kutaja madai ya msingi wanayotaka utatuzi wake kuwa ni pamoja na madereva wawe na mikataba bora na kupinga kitendo cha serikali cha kuwataka kwenda kusoma kila baada ya miaka mitatu wanapokwenda kuhuhisha leseni zao. 
 
Madai mengine ni ucheleweshwaji wa malori kwenye boda hususani ya Tunduma ambapo hukaa zaidi ya siku 26 licha ya kulipiwa kila kitu bandarini.
 
Salehe alitaja mengine kuwa ni sheria namba G 31 ya mwaka 2015 ambayo inazungumzia kuhusu faini ya Sh. 300,000 au kifungo cha miezi 21 kwa madereva wanapofanya makosa barabarani.
 
Alitaja madai mengine kuwa ni tamko la Mkufunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) alilolitoa Machi 31, mwaka huu kuwa, madereva wote waliopata leseni PSV sio mahiri hivyo hata wakirudi shule watapata alama 5.
 
Alisema madai mengine ni kukinzana kwa ratiba ya Mamlaka ya Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) pamoja na ile ya jeshi la polisi kuhusu mwendo na kufika eneo husika.
 
Pia alitaja dai la mwisho kuwa ni mikataba ambayo wamiliki wa magari wamekuwa hawawashirikishi wao.
 
Baada ya madai hayo kutajwa Waziri Kabaka alijaribu kujibu baadhi ya hoja huku zile ambazo zinawakereketa wahusika kama lile la kwenda kusoma na mikataba likibaki na kitendawili kilichosababisha, viongozi wa madereva hao kufunguka na kutaka majibu.
 
Kufuatia hali hiyo, Waziri Kabaka alilazimika kutangaza kuwa kwa niaba ya wizara ya uchukuzi, suala la kusoma limefutwa.
 
Pia aliwataka walipuuzie tamko la NIT kwa sababu halina nafasi wala halipo serikalini bali lilikuwa ni la mtu binafsi.
 
Kadhalika alisema hatma ya mikataba yao itapatiwa ufumbuzi kwenye kikao kinachotarajiwa kufanyika Jumamosi ijayo ambacho kitahusisha viongozi wa madereva na serikali.
 
Aliwaagiza wamiliki wa mabasi na malori kuhakikisha wanapofuatilia mikataba ya madereva wao, waongozane na wahusika na kuacha ubabaishaji.
 
Naye, Kamanda Kova alitangaza kuwa, kuanzia sasa suala la tochi zinazotumiwa barabarani na polisi limefutwa na kuwataka madereva wafuate sheria za usalama barabarani ili kuepuka ajali.
 
Kuhusu ‘mabao’ ya ovyo yanayofanya na trafiki barabarani ambayo madereva hao waliyalalamikia, Kamanda Kova aliwapa watu hao namba zake za simu ili wanapokamatwa wampigie.
 
Kova alitangaza kuwa kuanzia sasa kituo cha ukaguzi kitakachotumika ni kile cha mizani pekee.
 
ABIRIA WANENA
Mwanafunzi wa Kidato cha tano katika Shule ya Sekondari ya Weruweru, Doris Mayemba, amesemakuwa, wanafunzi 66 wa shule hiyo wamekwama kituoni hapo baada ya mabasi hayo kugoma.
 
Kuhusu upigwaji wa mabomu, Mayemba alisema kimewasababishia mshtuko na mwanafunzi mwezake Linda Salonga, alizirai lakini sasa anaendelea vizuri.
 
MBAGALA
Mbagala, hali ilikuwa ngumu baada ya polisi kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya madereva na abiria waliokusanyika kituo cha mabasi cha Mbagala Rangitatu.
 
Tukio hilo lilianza majira ya saa 3:15 asubuhi, baada ya kundi la madereva na wapiga debe kuwashusha watu waliopanda magari na pikipiki maarufu kama bodaboda waliokuwa wakitoa huduma ya usafiri.
 
Watu hao waliweka vizuizi vya mawe katika Barabara ya Kilwa, hatua ambayo ilisababisha msongamano wa magari.
 
Polisi ambao walitumia magari matatu na pikipiki nne walifika eneo hilo mara moja na kuanza kutupa mabomu na kusababisha madereva na abiria waliokuwa kwenye kituo hicho kukimbia hovyo.
 
Milio ya mabomu ilisikika kwa muda wa dakika 15 na kusababisha watu kukimbilia kwenye maduka ya jirani na Hospitali ya Zakhem kwa ajili ya kulinda usalama wao.
 
Polisi hao walionekana wakiranda barabarani kuhakikisha usalama wa eneo hilo unarejea.
 
Polisi walifanikiwa kudhibiti eneo hilo na vituo vingine vya Mbagala Kizuiani, Kipati, sabasaba na Mtoni kitu ambacho baadhi ya madereva wa magari madogo ya mizigo na pikipiki walitumia nafasi hiyo kuanza kubeba abiria waliosongamana kwenye vituo hivyo.
Hali katika kituo cha Tandika ilikuwa na ukimya kufuatia magari kutoonekana kituoni hapo,huku magari machache yanayokwenda maeneo ya Yombo yalionekana yakiendelea kutoa huduma ya usafiri.
 
Hata hivyo, mmoja wa dereva ambaye hakutaka kutaja jina lake, alisema wao hawakushiriki kwenye mgomo huo kutokana na magari yao kutotambuliwa na Sumatra.
 
“Sisi hatuhusiki na migomo kwa sababu hata Sumatra wanasema hawatutambui, tunaendelea kuwachukua abiria kama kawaida,” alisema dereva huyo.
 
BAJAJ, BODABODA, MALORI YANEEMEKA
Abiria walilazimika kutembea kwa miguu kutoka kituo cha Ubungo hadi Mbezi wakitafuta usafiri wa mikoani bila mafanikio.
 
Mgomo huo wa madereva ulizusha vurugu na ngumi kati ya abiria na kikosi cha kuzuia magari katika kituo cha Ubungo.
 
Wakiongea abiria Selina Elisante, akiwa na wanawe watano huku akibubujikwa na machozi alisema wametumia gharama kubwa kujinunulia mahitaji ambayo hayakuwapo.
 
Stephen Mdemo alisema kuwa matatizo ya mgomo yaliandaliwa na jeshi la polisi lilikuwa na taarifa na kuhoji kwa nini hatua hazikuchukuliwa na kuwatesa abiria bila sababu.
 
Hali hiyo ya mgomo iliwanufaisha waendesha bodaboda na bajaji ambapo walianzisha umoja wa aina yake kwa kupandisha nauli kati ya Sh. 1000 hadi Sh. 5000 kwa abiria mmoja.
 
Nauli  kutoka Tegeta Nyuki hadi Mwenge ilikuwa Sh. 5,000 na Kimara hadi Ubungo, Sh. 4,000.
Bodaboda ilitoza Sh. 4,000 kwa safari moja bila kujali umbali.
 
Viongozi wa Madereva waliomba msaada wa polisi kutoa ulinzi kwa magari yatakayosafirisha abiria kutoka jijini Dar es Salaam kwenda mkoani, jambo ambalo polisi halikulipa umuhimu wake mpaka pale majanga yalipotokea na kuanza kuchukua hatua ya kurusha mabomu yakutawanya wananchi.
 
Madereva hao wanapinga sheria za usajili inayowataka wakitaka kuongeza daraja kwenda chuoni kusoma kwa madai kuwa hawana uwezo kutokana na mishahara yao kuwa kidogo. Isitoshe,  wamiliki hao hawawezi kuwavumilia mpaka wamalize kozi, wanahofia kukosa kazi kwa mmiliki kuajiri dereva mwingine.
 
Athari ya mgomo huo ulisababisha wafanyakazi wengi kufika maeneo yao ya kazi wakiwa wamechelewa au kutofika kabisa huku wengi wakibebwa kwenye malori ya mchanga yaliyokuwa yakitoza nauli ya Sh. 1000 kutoka Mbezi hadi Ubungo. 
 
Wakati huo huo, abiria walijikuta katika wakati mgumu katika masuala ya usafiri na kujikuta wakitumia gharama kubwa. Anna Kilemba ambaye alikuwa anasubiri usafiri wa kwenda Posta, anasema kutokana na usafiri kuwa wa shida ilimlazimu kupanda gari aina ya NOAH ambapo alilipa Sh. 1,500. 
 
Hata hivyo baadhi ya abiria wakipanda gari ambazo zinatumika kubebea mizigo maarufu kwa jina la ‘Kirikuu’ kwa kutangaziwa nauli ya Sh. 1,000.
 
Baadhi ya watu ambao walikuwa wanapeleka chakula kwa wagonjwa hospitali ya Muhimbili walijikuta katika wakati mgumu huku wakichelewa kutokana na kukosekana kwa usafiri.
 
Amina abdallah alisema licha ya kuchelewa kufika hospitalini hapo lakini imemgharimu zaidi ya Sh.10,000 kulipia usafiri wa bodaboda wakati huwa anatumia Sh. 800.
 
PWANI
Abiria zaidi ya 1000 wa mabasi yaliyokuwa yakitoka mikoani kwenda kituo cha Ubungo Dar es Salaam,  walikwama katika kituo cha mabasi Maili moja mjini Kibaha baada ya kuhofia kupigwa kufuatia mgomo wa madereva.
 
Baadhi ya abiria walilsema kuwa pamoja na  mgomo huo kuisha baada ya mazungumzo kati ya madereva na serikali wameshindwa kusafiri kutokana na kuchoka na muda kuisha.
 
“Nipo hapa tangu asubuhi saa 12, hadi saa saba ndio tunaona magari yanaanza safari, sasa nimeshachoka na muda nao umeshaenda pia bajeti yangu hairuhusu kusafiri nimeshapunguza nauli kwa kununua chakula, alisema Said Haji abiria aliyekuwa katika kituo cha Mail moja mjini Kibaha.
 
Mmiliki wa magari ya Smart Bus yanayofanya safari zake kati ya Dar es Salaam-Tanga-Mombasa, Nuru Jumbe, alisema mgomo huo umewaathiri kwani gari lake moja lililokuwa kituo cha mabasi Ubungo ilipigwa mawe na  ilivunjiwa kioo cha mbele na hivyo kumlazimu kuipeleka gereji kwa gharama kubwa ambazo hakuzitegemea.
 
MWANZA
Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Baraka Konisaga, jana aligomewa na madereva wa mabasi ya kwenda mikoani katika kituo kikuu cha mabasi Nyegezi jijini Mwanza, baada ya kuwalazimisha kusitisha mgomo wao na kuanza safari.
 
Akizungumza na baadhi wasafiri, madereva na wamiliki wa baadhi ya mabasi hayo katika kituo hicho, alisema madereva wanapaswa kuanza safari kutokana na wamiliki kutotambua mgomo huo.
 
“Abiria ingieni ndani ya mabasi yenu kwa ajili ya kuanza safari, polisi jipangeni sawa kwa ajili ya ukaguzi na madereva waanze na safari…kuna abiria wenye matatizo mbali mbali hapa na kutakiwa kuwahi waendako, sasa safari ianze huku serikali ikizungumza na viongozi wenu,” alisema Konisaga.
 
Konisaga aliyefuatana na Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Japhet Lusingu, viongozi wa mamlaka ya usafiri wa nchi kavu na majini (Sumatra) mkoa na mkuu wa kikosi cha usalama barabarani mkoa wa Mwanza, alisema madereva hawana haki ya kugoma kutokana na wamiliki wa magari kutoutambua mgomo huo.
 
Miongoni mwa abiria walioshindwa kusafiri, Mwenge Soka, alisema wanashangazwa kwa kukatiwa tiketi hadi asubuhi, lakini wakifahamu mabasi hayo hayawezi kusafiri.
 
KIGOMA
Zaidi ya abiria 2000  walipigwa butwaa jana katika stendi mpya ya Masanga eneo la Manispaa ya Kigoma/Ujiji  bila kujua la kufanya baada ya madereva wa mabasi mbalimbali kugoma kutoa huduma hiyo.
 
Akizungumza , dereva wa basi la Saratoga linalofanya safari zake Kigoma hadi Dar es Salaam, Ositazi Ibrahimu (45) alisema wameunga mgomo wa nchi nzima baada ya viongozi wao wa Chama ch Madereva Tanzania kukamatwa  kwa madai ya kuwatetea madereva wote Tanzania.
 
Abiria Laila Rashid (30) aliyekuwa amepanda basi la Saratoga  kutoka Kigoma kuelekea Tabora, alisema alitakiwa aonane na daktari saa nane mchana lakini ameshindwa.
 
Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Madereva Mkoa wa Kigoma, Tunu Rashid, alisema  “tatizo kubwa ni mfumo wa serikali.
 
Naye Mwalimu Ezekieli Kanyangwa, ambaye ni abiria wa basi la Adventure lililokuwa likielekea Mpanda alisema kilichomshangaza wakati ameenda kukata tiketi hakuambiwa kuwa kuna mgomo.
 
Kanyangwa alisema hadi saa tano asubuhi nauli hawajarudishiwa na mgomo unaendelea hawajui la kufanya wala hakuna kiongozi yeyote aliyetoa taarifa kuhusiana na mgomo huo.
 
MTWARA
Abiria wa mabasi yanayoenda sehemu mbali mbali wameshindwa kusafiri kutokana na mgomo wa madereva kupinga amri ya serikali kuwataka kwenda kusoma.
 
Katika kituo cha mabasi Mtwara  idadi kubwa ya mabasi ya kwenda mikoani yakiwa yameegeshwa huku abiria wakiwa hawajui la kufanya ikiwa tayari walishalipia tiketi kwa ajili ya kusafiri.
 
Akizungumza kituoni hapo, Vaileti Nickolous ambaye alikuwa akisafiri kuelekea Dar es Salaam, alisema mgomo huo umewaathiri kutokana na wasafiri kupoteza muda na wengine walikuwa wanakwenda kwenye matatizo.
 
“Wengine wanawahi maofisini, wengine wanasafiri kibiashara..sasa kama mfanyabiashara amenunua biashara zake anatakiwa sasa akasafirishe na biashara yenyewe kama matunda, kwa mgomo kama huu lazima atapata hasara,” alieleza Violet.
 
MASASI 
Abiria waliokusanyika katika stendi kuu ya mabasi wilayani Masasi walisema mgomo huo umewaathiri ikiwemo mipango mbali mbali waliyojiwekea katika shughuli zao za kila siku.
 
Walisema wameshangazwa na madereva hao kukatisha tiketi kutoka kwa abiria wakati wakifahamu kuwa walikuwa na nia ya kufanya mgomo.
 
Juma Omari na Fatuma Justice kwa niaba ya abiria wengine wamesema kuwa wanasafiri kwenda Dar es Salaam lakini walipofika stendi walikuta abiria wengine wakiwa wamekusanyika makundi huku baadhi wakiwa wamekaa ndani ya magari wasijue la kufanya.
 
mwandishi wetu alishuhudia pia madereva wa pikipiki za miguu mitatu na zile bodaboda zikishiriki katika mgomo huo ambapo mji wa Masasi ulionekana kimya baada ya vyombo hivyo kutokuwapo barabarani na wakazi wa mji huo wakilazimika kutembea kwa miguu kwenda katika shughuli zao.
 
SONGEA
Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu, alipohojiwa kwa njia ya simu alisema kuwa tatizo hilo la mgomo wa madereva linafahamika na  tayari amekutana na kamati yake ya ulinzi na usalama kwa lengo la kuangalia tatizo lenyewe lilivyo kwa mkoa wa Ruvuma.
 
Meneja wa kampuni ya usafirishaji wa mabasi ya Super Feo Christian Sanga alipoulizwa sababu ya kukatisha tiketi wakati mabasi hayatasafiri, alisema mgomo wa madereva ni wa kihuni kwa kuwa hawakupewa taarifa kama madereva wao hawatafanya kazi.
 
LINDI
Abiria waliofika kituo cha mabasi mjini hapa walipigwa na butwaa baada ya kutokuta gari hata moja kituoni.
 
Kaimu Afisa wa Sumatra mkoani Lindi, Mwasi Christian, alipotakiwa kutoa ufafanuzi kuhusu mgomo huo, alisema yeye si msemaji wa mamlaka.
 
Abiria waliokwama kusafiri waliiambia NIPASHE kuwa wamesikitishwa na kitendo hicho huku wakiwatupia lawama matajiri kwa kushindwa kuwapa haki zao za msingi madereva wao.
 
MOROGORO
gari ndogo za abiria maarufu kama daladala zinazofanya safari zake ndani ya mkoa wa Morogoro ziligoma kwa muda wa saa kumi jana na kusababisha abiria kupata adha ya usafiri huku wengine wakilazimika kupanda pikipiki na magari ya wazi ili kufika maeneo yao ya kazi na shuleni.
 
Mgomo huo ulioanza saa 12 asubuhi hadi kufikia saa 9 alasiri yalipoanza kufanyakazi kama kawaida.
 
Akizungumzia hilo Kamanda wa Polisi mkoani hapa Leonard Paulo alisema, jeshi hilo linawashikilia watu saba kwa tuhuma za kufanya fujo na kuleta uvunjifu wa amani mkoani hapa.
 
Kamanda huyo alisema watu hao walikamatwa jana aprili 10, saa 5 asubuhi katika eneo la Kihonda wakijaribu kuwazuia madereva wenzao wa magari na pikipiki kuacha kuwabeba abiria waliokuwa vituoni kwa madai kuwa wanaendeleza mgomo huo hadi hapo watakapopata suluhu.
 
MBEYA
Mgomo wa madereva uliokuwa umepangwa kufanyika jana nchi nzima haukufanyika kama ilivyokusudiwa na badala yake shughuli za usafirishaji ziliendelea kama kawaida katika maeneo yote.
 
mwandishi wetu ametembea vituo vyote vya mabasi na kushuhudia magari ya kusafirisha abiria na mizigo yakiendelea na shughuli zake kama kawaida.
 
Katika Kituo Kikuu cha Mabasi jijini Mbeya, mabasi ya kwenda mikoani yaliondoka kuanzia saa 12:00 asubuhi kuelekea maeneo mbalimbali kulingana na ratiba walizopangiwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Mjini na Nchi Kavu (Sumatra).
 
*Taarifa hii imeandaliwa na Romana Mallya, Moshi Lusonzo, Beatrice Shayo,
Efracia Masawe, Agnes Temu, Margaret Malisa,Pwani Hamisi Abdelehemani, Masasi, Emmanuel Lengwa, Mbeya, Joctan Ngelly Kigoma, Daniel Mkate, Mwanza, Juma Mohamed, Mtwara, Gideon Mwakanosya, Songea, Said  Hamdani, Lindi, Christina Haule, Morogoro

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni