MMILIKI WA BLOG HII

MMILIKI WA BLOG HII
TANGAZA NASI MATANGAZO YA KIJAMII BURE KUPITIA BLOG HII

Jumamosi, 11 Aprili 2015

Gaweni nakala katiba pendekezwa msizifungie makabatini'.

                Waziri wa Katiba na Sheria, Dk.Asha Rose Migiro

Baraza la Vyama vya Siasa limevitaka vyama vyote vilivyopata mgawo wa nakala ya Katiba inayopendekezwa kuwagawia wanachama na wananchi badala ya kuendelea kuzifungia kwenye makabati ya vyama.
 
Mwenyekiti wa baraza hilo, Peter  Mziray, akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, alisema serikali ilitoa nakala ya Katiba hizo ili vyama viweze kuwagawia wanachama wake ambao watapata fursa ya kusoma na kufanya tathmini kulinganisha na Katiba ya sasa.
 
“Vyama vikifungia kwenye makabati nakala za katiba inayopendekezwa vitakuwa haviwatendei haki wananchi na lengo la serikali litakuwa halijafanikiwa,”alisema.
 
Mziray ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha APPT Maendeleo, alisema wananchi wakisoma Katiba inayopendekezwa wataweza kufanya maamuzi sahihi siku ya kupiga kura ya maoni ya kuikubali au kuikataa katiba hiyo.
 
Alisema APPT Maendeleo imeanza kusambaza nakala hizo katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam ili kuonyesha mfano kwa vyama vingine.
 
Vyama vyenye wabunge vilipewa nakala 15,000 za Katiba inayopendekezwa na visivyokuwa na wabunge nakala 5,000.
 
Serikali ilianza kusambaza nakala milioni mbili za Katiba inayopendekezwa nchini kote Februari mwaka huu ili kuwawezesha wananchi kuisoma na kushiriki katika kura ya maoni.
 
Waziri wa Katiba na Sheria, Dk.Asha Rose Migiro akisambaza katiba hizo, alisema zipo kata zaidi ya 3,800 nchini kote na lengo la Serikali ni kusambaza nakala 300 katika kila kata ambazo zitasambazwa kwenye vijiji, vitongoji na mitaa kupitia Ofisi za Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri za Miji, Manispaa na Majiji.
 
Kuhusu taasisi za elimu na dini, Waziri Migiro alisema Serikali imesambaza nakala 658,400 kwa taasisi za elimu, dini, vyama vya siasa na asasi za kiraia na kuwa usambazaji huo utaanza hivi karibuni.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni